Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES
SALAAM
MWANASOKA bora wa zamani wa
dunia, Luis Figo ameahidi
burudani nzuri ya soka kesho
Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam
wakati magwiji wa Real Madrid
ya Hispania watakapomenyana na
magwiji wa Tanzania katika
mchezo wa kirafiki.
Akizungumza na Waandishi wa
Habari mchana huu katika hoteli
ya Southern Sun, Dar es Salaam,
mshindi huyo wa Ballon d’Or
mwaka 2000, aliyestaafu Mei 31
mwaka 2009, amesema kwamba
Watanzania watafurahia kazi yake
uwanjani kesho.
Figo aliyepiga tuzo mbili
mfululizo mwaka 2000,
Mwanasoka Bora Ulaya na Dunia,
amewaomba wapenzi wa soka
Tanzania kujitokeza kwa wingi
kesho kushuhudia burudani.
“Ni mara yangu ya kwanza kuja
Tanzania, nimekwishatembea
nchi kadhaa Afrika, nimefurahi
kuja hapa, naipenda Afrika.
Natarajia mchezo mzuri kesho,
hata kwa wapinzani wetu pia, kitu
muhimu ni kwamba FIFA
imefurahia tukio hili,”alisema
Figo.
Kwa upande wake, mwanasoka
bora wa Oceania mara mbili
1995 na 1998, Christian
Karembeu aliyeshinda Kombe la
Dunia na Ufaransa mwaka 1998,
amesema kwamba atampa pasi
nyingi kesho Figo afanye vitu
vyake.
Beki wa zamani wa kimataifa wa
Hispania, Fernando Sanz Duran ni
miongoni mwa wanasoka watatu
waliowika Real Madrid muongo
uliopita waliofika jana usiku,
ambaye pia alikuwepo kwenye
mkutano wa leo.
“Nimefurahi kuja Tanzania, ni
mara yangu ya kwanza,
Watanzania watarajie burudani
nzuri kutoka kwetu na wapinzani
wetu,”alisema Sanz huku
akimgusa begani, kocha Msaidizi
wa Magwiji wa Tanzania, Jamhuri
Kihwelo ‘Julio’.
Mshambuliaji wa zamani wa
kimataifa wa England, Michael
Owen aliyeshinda tuzo ya
mchezaji bora chipukizi Kombe la
Dunia mwaka 1998 Ufaransa,
anatarajiwa kuwasili katika kundi
la mwisho la Magalactico hao
jioni ya leo.
Mkurugenzi wa makampuni ya
Tanzania Sisi ni Nyumbani (TSN),
Farough Baghozah ambao ndiyo
wanawaleta magwiji hao nchini,
amesema maandalizi yote
yamekamilka na Watanzania
wajitokeze kwa wingi Taifa kesho.
Magalactito wa Real wamefikia
katika hoteli ya Ladger Plaza,
Bahari Beach wakati timu ya
Tanzania imeweka kambi
Kariakoo, Dar es Salaam
kikiendelea na mazoezi Uwanja
wa Taifa.
Kikosi hicho kinaundwa na
makipa maarufu waliowahi
kuwika nchini, Mwameja
Mohamed na Manyika Peter,
mabeki Nsajigwa Shadrack,
Mecky Mexime, Boniface Pawasa,
John Mwansasu,
Abubakar Kombo, George
Masatu, Habib Kondo,
Viungo Athumani China, Shaaban
Ramadhani, Salvatory Edward,
Sabri Ramadhani ‘China’, Yussuf
Macho, Abdul Mashine, Abdul
Maneno, Mao Mkami, Steven
Nyenge, Madaraka Suleiman,
Akida Makunda na Mtwa Kihwelo.
Washambuliaji ni Monja Liseki,
Iddi Moshi, Dua Said, Emmanuel
Gabriel, Said Maulid, Thomas
Kipese, Nasor Mwinyi ‘Bwanga’,
Edibilly Lunyamila, Mohamed
Hussein ‘Mmachinga’, Clement
Kahbuka,
Madaraka Suleiman na Akida
Makunda.
Benchi ka Ufundi, ni Kocha
Charles Boniface Mkwasa ‘Master’
na Wasaidizi Freddy Felix Minziro
na Jamhuri Kihwelo ‘Julio’, Daktari
Mwanandi Mkwankemwa na
viongozi Mtemi Ramadhani,
Hassan Mnyenye, Omar Gumbo
na Hamisi Kisiwa.
Katika ziara hiyo, pamoja na
kucheza mchezo wa kirafiki na
kikosi maalum cha wachezaji
nyota wa Tanzania Agosti 23, pia
watafanya utalii katika vivutio
mbalimbali, ikiwemo kupanda
mlima Kilimanjaro. |