Wednesday, October 22, 2014
|
Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
BAADA ya mechi nne mfululizo za nyumbani
katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara,
Simba SC itacheza mechi yake ya kwanza
ugenini mwishoni mwa wiki.
Simba SC itacheza na Prisons Uwanja wa
Sokoine mjini Mbeya Jumamosi, Ikitoka
kutoa sare nne katika mechi zote za
mwanzo, 2-2 na Coastal Union, 1-1 na Polisi
Moro, 1-1 na Stand Unted na 0-0 na Yanga
SC.
Katika Ligi yetu, nyumbani ni sehemu nzuri
ya kuvuna pointi kuliko ugenini, hususan
timu za Dar es Salaam zinaposafiri mikoani
na kwenda kukutana na viwanja vyenye hali
isiyo nzuri sana katika eneo la kuchezea.
Sasa Simba SC ndiyo wanaingia katika
wakati huo, kwani baada ya mechi na
Prisons Jumamosi, wiki inayofuata
watakuwa Uwanja wa Jamhuri, Morogoro
kumenyana na Mtibwa Sugar Novemba 1,
kabla ya kurejea tena Dar es Salaam
kucheza na Ruvu Shooting Novemba 9.
Huo utakuwa mchezo wa mwisho kabla ya
mapumziko marefu ya karibu mwezi mzima
kupisha Kombe la Mataifa ya Afrika
Mashariki na Kati, CECAFA Challenge na
michuano ya vijana ya Kombe la Uhai,
inayohusisha klabu za Ligi Kuu hadi
Desemba 26 ligi hiyo itakaporejea tena.
Simba SC haijashinda mechi kati ya nne
ilizocheza nyumbani na katika mechi zake
tatu zijazo, mbili itacheza ugenini tena dhidi
ya timu ambazo zinapokuwa nyumbani
kwao, hushinda mara nyingi.
Tayari kuna shinikizo la mashabiki kutaka
timu ishinde baada ya sare hizo nne za
nyumbani- na bahati mbaya Simba SC
inakwenda kwenye mchezo mgumu zaidi.
Kipa Ivo Mapunda bado hajapona na
anahitaji wiki mbili zaidi kabla ya kuanza
mazoezi taratibu, Hussein Sharrif ‘Casillas’
naye si wa kumtarajia mwaka huu kucheza-
maana yake klabu itacheza mechi hizo ikiwa
na kipa mmoja tu, Peter Manyika.
Huyo ni wa kumuombea naye asiumie na
wala asipate adhabu ya kumzuia kucheza-
wakati huo huo wachezaji wengine majeruhi
akina Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Miraj
Adam, Nassor Masoud ‘Chollo’, Paul
Kiongera, Jonas Mkude na Amisi Tambwe
mustakabali wao bado haueleweki.
Wazi mashabiki wa Simba SC wanatakiwa
kushikamana sana na timu yao kwa wakati
huu mgumu, wakijua hali halisi kwamba
wapo katika kipindi kigumu cha mpito. |
|
Wachezaji wa Simba SC watakuwa na mechi
mfululizo za ugenini kuanzia wikiendi hii |
0 comments:
Post a Comment