Saturday, August 23, 2014

Panga pangua, hii ndio Yanga mpya

HII ni siri usimwambie mtu yeyote, uchune nayo hivyo hivyo kwa vile bado Marcio Maximo hajaweka wazi kikosi chake cha kwanza lakini tathmini ya Mwanaspoti imekibaini. Kwa mujibu wa mazoezi yaliyofanyika Dar es Salaam na hapa Pemba jumlisha na mechi ya kirafiki waliyocheza, ‘First Eleven’ ya Yanga itakuwa kama ifuatavyo; Kipa ni Deo Munishi ‘Dida’ kama kawaida na Juma Abdul atacheza beki ya kulia. Kushoto ni Oscar Joshua lakini Edward Manyama na Amos Abeil anaocheza nao nafasi moja ni hatari sana, Maximo anaweza akawatumia kwa kuchanganya kulingana na timu pinzani. Beki ya kati ni Kelvin Yondani ‘Vidic’ na Nadir Haroub ‘Cannavaro’, kiungo mkabaji ni Mnyarwanda Mbuyu Twite na kiungo mshambuliaji ni Hassan Dilunga. Panga pangua Mbrazili Andrey Coutinho atacheza winga ya kushoto na Mnyarwanda Haruna Niyonzima atacheza winga ya kushoto, mastraika wa kati ni Mrisho Ngassa anayecheza kama kiungo nyuma ya Genilson Santos Santana ‘Jaja’. Kwenye nafasi za mbele, kiungo, winga na straika mambo yanaweza kubadilika kulingana na aina ya timu pinzani watakayocheza nayo. Kwani wachezaji kama Simon Msuva anaweza kutumika kucheza winga ya kulia kama anataka timu icheze kwa kasi zaidi, Jerry Tegete, Hamis Kiiza raia wa Uganda, Said Bahanuzi na Hussein Javu nao wanaweza kumpeleka Ngassa pembeni, kama atataka kucheza mpira wa kutulia. Maximo amesisitiza kuwa katika mechi hizi za majaribio, anataka kuwatumia wachezaji wote ili awaone na ndivyo anavyowapa nafasi. Ametengeneza ‘First Eleven’ mbili ambazo huchuana zenyewe kwa wenyewe na hao ndiyo watatoa kikosi halisi cha kwanza ambacho mwenyewe hajakiweka wazi. “Kwa sasa nampa kila mchezaji nafasi ya kucheza, lengo ni kuwaona namna wanavyocheza na muunganiko wa kombinesheni ipi inakubali kupata kitu fulani kulingana na mechi,” alisema Maximo. Maximo alitumia muda wa takribani robo saa akizungumza na wachezaji na baadaye walifanya mazoezi ya kukimbia na baadaye mafupi ya kucheza mpira. Katika mazoezi hayo, kiungo Hassan Dilunga, alishindwa kufanya mazoezi na wenzake kwani alikuwa anasikia maumivu kwenye kidole cha mwisho cha mguu wa kulia kwani alijitonesha kwenye mechi ya juzi Alhamisi na Chipukizi. Credit mwanaspoti

Kusoma habari nyingine BONYEZA HAPA 

0 comments:

Post a Comment