Monday, August 25, 2014

BAADA YA KIPIGO KIMOJA NA DROO MOJA KOCHA VAN GAAL AFUNGUKA MAZITO

KOCHA Mkuu wa Manchester United, Louis van Gaal amesema itakuwa ni muujiza mkubwa kwa timu hiyo kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu England msimu huu. Mdachi huyo ameilinganisha United ya sasa na Bayern Munich ya mwaka 2009 wakati alipokuwa akiinoa timu hiyo iliyokuwa na kikosi kilichokuwa na kasoro nyingi. Hata hivyo, Van Gaal akamaliza ligi msimu huo kwa kunyakua Ubingwa wa Bundesliga, kitu ambacho haoni kama kitaweza kujirudia kwa sasa akiwa na cha United. Wasiwasi wa Van Gaal umeibuka baada ya wiki iliyopita kuchapwa na Swansea City nyumbani Old Trafford katika mchezo wao wa kwanza wa Ligi Kuu England na kikosi chake jana Jumapili kilitarajia kumenyana na Sunderland kwenye ligi hiyo. Alipoulizwa kama aanze kutazamwa kiwango chake kwenye msimu wa kwanza au wa pili klabuni hapo, Van Gaal alijibu: “Siku zote hiyo ndiyo inakuwa kesi kubwa. Kitu ambacho kimenipa uzoefu ni kwamba nilikuwa bingwa Barcelona na Bayern, hivyo inawekana ila ni ngumu sana. “Nilipokwenda Bayern Munich kikosi kilikuwa hovyo. Kitu ambacho tulikifanya hadi mwisho wa msimu kilikuwa ni muujiza. Hapa Man United pia kikosi hakijatengemaa. Kuna namba 9 watano na namba 10 sita. Hatuna mabeki.” Alipoulizwa kama itakuwa muujiza kwa United kutwaa taji la Ligi Kuu England msimu huu, Van Gaal alisema: “Ndiyo, nadhani ni hivyo. Sawa siku zote inawezekana, lakini itakuwa ngumu sana.” credit mwanaspoti

0 comments:

Post a Comment