| SIMBA kila kona nchini wanashangilia baada ya
kumsainisha straika machachari mwenye
mkataba na Yanga, Emmanuel Okwi. Lakini
Mwenyekiti wa Yanga,Yusuf Manji, ameibuka na
kutoa msimamo mkali kwa kusisitiza kwamba
mchezaji huyo hatacheza Msimbazi.
Manji aliyeonekana na uso wa furaha wakati
wote wa mkutano wake na waandishi wa habari
akiambatana na Makamu wake Clement Sanga,
alisisitiza kwamba Yanga haiwezi kuwa chini ya
mchezaji mmoja na kwamba hawajawahi
kumuacha Okwi.
Alisema kwamba wamemfungulia mashtaka ya
kinidhamu TFF na hata katika orodha yao ya
wachezaji wa kigeni waliopelekwa TFF jina la
Okwi limo wakisubiri hatma ya kesi
waliyoifungua.
“Siku zote tumekuwa tukiwaheshimu hawa
jamaa zetu, mtamkumbuka mara kadhaa
nimekuwa nikiwapongeza hata wanapoifunga
timu yangu, tumekuwa tukiwasajili wachezaji
wengi wa Simba kama Kaseja (Juma), Yondani
(Kelvin) lakini hatukuwa tunawasajili wakati
wana mikataba tunasubiri mpaka mikataba yao
inapomalizika,”alisema Manji.
“Yanga hatuna desturi ya kulalamika
waliondoka Kavumbagu (Didier) na Domayo
(Frank) kwenda Azam hatukulalamika kwa kuwa
utaratibu ulifuatwa na hata hili hatulalamiki
kwa kuwa tunajua tunachokifanya, Yanga
hatujamuacha Okwi, ni mchezaji wetu.
“Inashangaza sana inawezekanaje mtu akawa na
ugomvi na mkewe wakati huohuo kuna mtu
mwingine anajitokeza kusikojulikana na
kutangaza kufunga ndoa halali na mkeo,
unaweza kujiuliza hawa watu wamekutana na
kupatana wakati gani, linatutia shaka hili.”
Manji alisema kwa kuwa tayari wameshafungua
kesi ya kwanza ambayo kabla ya kujibiwa
mchezaji husika ameongeza kosa lingine, sasa
Yanga imewasilisha TFF mashtaka mengine
ambayo sasa itawajumuisha Okwi, Simba na
wakala wa mchezaji.
Katika kesi hiyo sasa pande hizo tatu zitatakiwa
kuilipa Yanga kiasi cha Dola 500,000
(Sh825mil).
“Nina uwezo wa kuwanunua wachezaji wote wa
Simba pamoja na kocha wao Phiri (Patrick) na
kuwazuia wasicheze ligi wakae pale Gymkhana
wachezee mpira na kulala, lakini nikifanya
hivyo watu watalalamika Manji anaharibu
mpira.
“Najua kwamba mishahara ya wachezaji wangu
wa Yanga ya miezi miwili pale Simba inawalipa
wachezaji wao wote mwaka mzima, tunataka
kuona TFF inawafungia Okwi na Simba tunatoa
siku saba kujua hatma ya hilo ikishindikana
hapo tutaenda Fifa na CAS (mahakama ya
michezo),”alisisitiza Manji.
TFF yamtambua Okwi Yanga
TFF kupitia kwa Katibu wake Mkuu, Celestine
Mwesigwa, amethibitisha kwamba ofisi yake
haina mamlaka ya kutoa kibali chochote
maalum cha kumpeleka Okwi kuichezea Simba
ambapo kwa sasa bado wanamtambua mchezaji
huyo kuwa ni mali ya Yanga.credit mwanaspoti |
0 comments:
Post a Comment